Thursday, 1 March 2018

SHAIRI KWA WAKRISTO



MATHAYO 5 : 14 -16
Jukumu ninajitwika, kushukuru wetu mu’mba,
Kutuwezesha kufika, kwenye takatifu jumba,
Nadhani ninasikika, nanyi nyote kwenye jumba,
Mimi hapa nimefika, maadili kuyalumba
Tusiwashe zetu taa, halafu tufunikie,

Katika mathayo tano, anza arobatashara,
Pitia kumi na tano, fikia sitatashara,
Yatoa mwema mfano, wakutuweka imara,
Naomba tuwe  mifano, tuyaache masihara,
Tusiwashe zetu taa, halafu tufunikie,

Twafananishwa na mji, ul’ojengwa mlimani,
Ni wengi watazamaji, huuona duniani,
Jalali hutuhitaji, tuwe mwanga maishani,
Aidha hutuhitaji, tumulike hadharani,
Tusiwashe zetu taa, halafu tufunikie,

Ikiwa tumeokoka, twonyeshe wokovu wetu,
Tuweze kuheshimika, katika maisha yetu,
Na tuwe wa kuigika, katika matendo yetu,
Tuwe wa kutajika, kwa wema ulonyumetu,
Tusiwashe zetu taa, halafu tufunikie,

Tusiwe watu wa chuki, tusije dharauliwa,
Tufaane kwenye dhiki, mola ataabudiwa,
Tuombeane riziki, na tena kubarikiwa,
Tusiunge ufasiki, kwani tumeteuliwa,
Tusiwashe zetu taa, halafu tufunikie,

La Mola husema buku, tusiwe wa kugawanya,
Tusiwe wenye udaku, na wenzetu kuwasinya,
Tusiwe watu wa chuku, midomo ya kusengenya,
Tuzipige marufuku, akili za kudanganya,
Tusiwashe zetu taa, halafu tufunikie,

Naomba mnipe mwanya, niende nyumbani kwangu,
N’ambie babu na nyanya, na hata wazazi wangu,
Liwapasao kufanya, ili waitwe wa Mungu,
Machache nimewakanya, tii ushauri wangu,
Tusiwashe zetu taa, halafu tufunikie.

SHUKURANI
Malenga Marc Karash

SHAIRI KUHUSU VIPAJI



KIPAJI NI NGUVU
Kabla jimbi kuwika, nashukuru wetu mu’mba,
Kutuwezesha kufika, kwenye takatifu jumba,
Nadhani ninasikika, nanyi nyote kwenye jumba,
Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani,

Vipaji vipaji kaka, hupeanwa naye mu’mba,
Vipaji vya kutajika, kucheza ama kuimba,
Vingine vya kusifika, kuchora ama kulumba,
 Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani,

Mola ‘liona mwafaka, nisiitwe ombaomba,
Kipaji akanitwika, maishangu kuyapamba,
Mashairi naandika, Januari hadi Disemba,
 Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani,

Shairi nikiandika, linakuwa kama dumba,
Mamia waelimika, nakwacha zao kasumba,
Sasa ni wakuigika, hakika si kujigamba,
Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani,

Nasema leo hakika, kama wajua kuimba,
Uimbe ukisikika, usiimbe kwenye chemba,
Sababu ukisikika, sifa zako zitatamba,
Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani,

Nasema leo hakika, kama wewe ni Lomba,
Ama ulibahatika, na unajua kulumba,
Onekana na sikika, ukilomba ukilumba,
 Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani,

 Kalamu nimeiweka, nakoma usemi wangu,
Sasa imeeleweka, kwenye aridhi na mbingu,
Kila mtu ameshika, kipaji toka kwa Mungu,
Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani.

SHUKURANI
 Malenga Marc Karash.

SHAIRI KWA WOTE



CHANGAMOTO ZA MAISHA
Safari nimeshafunga, katika maisha yangu,
Mbele mbele ninasonga, nifikie ndoto zangu,
Hasimu wakinitenga, natuliza moyo wangu,
 Changamoto za maisha, haziui ndoto zangu,

Tangu nikiwa mchanga, maisha ni dungudungu,
Riziki ninaidanga, huku nikiomba Mungu,
Wale wananisimanga, wasiue ari yangu,
 Changamoto za maisha, haziui ndoto zangu,

Ukata umebiringa, wengi wa umri wangu,
Ndoto zao kabananga, wakabaki na uchungu,
Lakini nauchabanga, hautanifunga pingu,
 Changamoto za maisha, haziui ndoto zangu,

Matatizo yamenisonga, katika maisha yangu,
Rafiki wananibonga, watangaza siri zangu,
Wengine wananikenga, wachanganye bongo zangu,
Changamoto za maisha, haziui ndoto zangu,

 Hela zanipiga chenga, sijalipa karo yangu,
Mwenye nyumba ‘meifunga, na kupa wake ufungu,
Leo nakoma kupanga, nisake nyumbani kwangu,
 Changamoto za maisha, haziui ndoto zangu,

Beti zangu nimefunga, niende nyumbani kwangu,
Ndugu nimeshawagunga, katika hayo mafungu,
Nangoja mvue kanga, muige msemo wangu,
Changamoto za maisha, haziui ndoto zangu.

SHUKURANI
Malenga Marc Karash.

SHAIRI KWA MPENZI



MPENZI WANGU
Tangu nilipokuona, ninahisi nina deni,
Kuna jambo sijanena, laninyima burudani,
Najaribu kulinena, sasa mara elfeni,
Na leo nimekazana, nikwambie hadharani,

Nimeona wasichana, wengi toka utotoni,
Kama wewe sijaona, kipenzi hurulaini,
Picha yako naiona, usiku usingizini,
Na leo nimekazana, nikwambie hadharani,

Umbo limebabatana, hasa pale kifuani,
Nitaishi kulighana, siku zangu maishani,
Na sura yaambatana, na rangi kote mwilini,
Na leo nimekazana, nikwambie hadharani,

Nywele zako umechana, zinafika mabegani,
Usemi wako mwanana, na tabasamu usoni,
Utulivu wa kinena, yote hayo buruhani,
Na leo nimekazana, nikwambie hadharani,

Mikono yako kimwana, misafi tena laini,
Nyuma wapendeza sana, watia fisi mbioni,
Na macho ya kiborana, yang’aa bila miwani
Na leo nimekazana, nikwambie hadharani,

Muda wangu wa kunena, umefika ukingoni,
Ni mengi sijayanena, kutoa  yalo moyoni,
Sababu wewe kimwana, penzi lako li moyoni,
Na leo nimekazana, nikwambie hadharani,

SHUKURANI
Malenga Marc Karash

SHAIRI KWA WANAFUNZI KIDATO CHA KWANZA.



KURUNZI BORA

Hamjambo wanafunzi, karibu hapa shuleni,
Hivi leo kiburunzi, siku yenu ugenini,
Nimekataa kihunzi, nawa’mbia hadharani,
Iliyo bora kurunzi, ni kusoma upilini,

Mmeviruka viunzi, tangu pale msingini,
Mtawawahi wapenzi, mkiwa hapa shuleni,
Mtasimulia tenzi, lakini mkumbukeni,
Iliyo bora kurunzi, ni kusoma upilini,

Myakumbuke majonzi, ya wazazi viamboni,
Wengine wakurugenzi, wengine wa mashambani,
Lakini wanayaenzi, masomo ya upilini,
Iliyo bora kurunzi, ni kusoma upilini,

Hapa tuna wakufunzi, walimu ‘toka vyuoni,
Aidha tuna walinzi, mliopata langoni,
Pia tuna wanafunzi, watakao wa’mbieni,
Iliyo bora kurunzi, ni kusoma upilini,

Nidhamu na muienzi, musiruke adhabuni,
Sikio lisife ganzi, ushauri sikizeni,
Leo tuanze utenzi, wa kufaidi mwishoni,
Iliyo bora kurunzi, ni kusoma upilini,

Kalamu yapiga kwenzi, nakudai niacheni,
Sikuifunga tanzi, itabidi nikomeni,
Isije leta kitanzi, nikidhani ni utani,
Iliyo bora kurunzi, ni kusoma upilini,

SHUKURANI
Malenga Marc Karash

HADITHI YA KUSISIMUA

ANN NA MUTUVIE Jina lake ni Ann. Sura anayo ndio, umbo analo ndio pia tabasamu lake lingemvutia kila mtu kwenye gari waliyoisafiri. M...