Thursday, 1 March 2018

SHAIRI KUHUSU VIPAJI



KIPAJI NI NGUVU
Kabla jimbi kuwika, nashukuru wetu mu’mba,
Kutuwezesha kufika, kwenye takatifu jumba,
Nadhani ninasikika, nanyi nyote kwenye jumba,
Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani,

Vipaji vipaji kaka, hupeanwa naye mu’mba,
Vipaji vya kutajika, kucheza ama kuimba,
Vingine vya kusifika, kuchora ama kulumba,
 Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani,

Mola ‘liona mwafaka, nisiitwe ombaomba,
Kipaji akanitwika, maishangu kuyapamba,
Mashairi naandika, Januari hadi Disemba,
 Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani,

Shairi nikiandika, linakuwa kama dumba,
Mamia waelimika, nakwacha zao kasumba,
Sasa ni wakuigika, hakika si kujigamba,
Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani,

Nasema leo hakika, kama wajua kuimba,
Uimbe ukisikika, usiimbe kwenye chemba,
Sababu ukisikika, sifa zako zitatamba,
Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani,

Nasema leo hakika, kama wewe ni Lomba,
Ama ulibahatika, na unajua kulumba,
Onekana na sikika, ukilomba ukilumba,
 Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani,

 Kalamu nimeiweka, nakoma usemi wangu,
Sasa imeeleweka, kwenye aridhi na mbingu,
Kila mtu ameshika, kipaji toka kwa Mungu,
Kipaji changu ni nguvu, na kurunzi maishani.

SHUKURANI
 Malenga Marc Karash.

1 comment:

HADITHI YA KUSISIMUA

ANN NA MUTUVIE Jina lake ni Ann. Sura anayo ndio, umbo analo ndio pia tabasamu lake lingemvutia kila mtu kwenye gari waliyoisafiri. M...