Sunday, 3 November 2019

HADITHI YA KUSISIMUA


ANN NA MUTUVIE
Jina lake ni Ann. Sura anayo ndio, umbo analo ndio pia tabasamu lake lingemvutia kila mtu kwenye gari waliyoisafiri. Mutuvie alikaa kimya na kujifanya hayaoni hayo. Ann alishangaa Mutuvie ni mvulana aina gani, imani yake ni gani na wapi akaazima hisi zake za kiume.  Itakuwaje wamesafiri takribani kilomita tatu sasa bila ya kusemezana chochote. Alitamani gari hili lingekuwa na kiti cha ziada angehamia pale amwache mvulana wetu. Alifungua begi yake ya mkononi  iliyokuwa juu ya mapaja yake huku ameikumbatia tumboni pake. Alitoa wanja na kioo cha kiduara chenye ngozi ya rangi ya kijani. Alipangusa pangusa mboni zake huku akijitazama kwenye kioo na baadaye kurudisha bidhaa zake. Hakutumia wanja. Alitazama juu kidogo kama anayewaza jambo Fulani. Alijivuta nyuma kitini na kuvuta sketi yake fupi kujaribu kuficha mapaja yake yaliyoachwa wazi. Alikuwa amevalia mini sketi ya rangi ya samawati na shati nyeupe iliyoshindwa kuficha rangi nyekundu ya kanchiri. Kichwani alisongwa mtindo wa sokota.

Kwa upande mwingine, Mutuvie alijifanya ametulia ila alikuwa na mshangao na wasiwasi mwingi. “panya anafanya nini ndani ya begi langu? Alipitia wapi kuingia humo? Nimesafiri naye kwa muda gani?” Hayo ni baadhi ya maswali aliyokuwa anajiuliza kijana Mutuvie. Kusema ukweli, Mutuvie alivutiwa na urembo wa Ann. Alichukua karibu dakika ishirini tangu gari ling’oe nanga akifikiria ataanza vipi kumsemeza Ann. Alikuwa kwenye kipindi cha kuuguza majeraha aliyopata baada ya kupewa talaka na mpenzi wake wa muda mrefu baada ya muhula wa mwisho chuoni. Fursa hii, aliiona mwafaka kutibu majeraha yake ya kimapenzi. Baada ya dakika hizo ishirini, alipata wazo. Aliamua kuchukua rununu yake, aandike ujumbe kuhusu hisia zake kwa Ann kisha amwache Ann asome kwenye kiwaa cha simu hiyo. Alistaajabu ya Musa alipofungua begi lake la begani lenye rangi ya udongo. Hakustaajabishwa na usafi wa suruali lake jeusi  la kiofisi wala usafi wa shati lake jeupe la kiofisi bali alistaajabishwa na panya mkubwa kimo cha paka aliyekuwa anatawala ndani ya begi lake. Aliharrakisha kufunga begi hilo. Hakutaka Yule panya atoke kwanza ili asijiaibishe kwa Ann na pili asiwashtue abiria wengine.  Alifunga begi lake na kukaa kimya hata hayaoni haya yote Ann anayoyafanya.

Mutuvie anakumbuka tu akimwambia Ann “safari salama.” Njiani alipanda na kushuka, kuelekea nyumbani kwao. Alikuwa na majukumu mawili mbele yake. Kwanza, ingebidi aeleze wazazi wake kumhusu panya aliye ndani ya begi lake. Angetaka  yeye na wazazi wake wasaidiane kufikiri sababu ya panya kuingia begini mle. Pili, angeeleza wazazi wake na mwingine yeyote kuhusu kufuzu kwake katika mitihani yote pale chuoni. Alikuwa katika orodha ya waliotarajiwa kuhitimu katika shahada ya kwanza wiki iliyofuata. Huo ndio ujumbe uliomfanya kuelekea nyumbani.

Mutuvie alipofika kwenye lango la boma yao, mambo yalibadilika. Ingawaje yeye sio mgeni, mbwa wao hubweka dhidi ya mtu yeyote apitiaye lango la boma hiyo. Siku hiyo hakubweka wala hakuonekana. Jambo hili lilimtia Mutuvie wasiwasi. Alipiga hodi asikaribishwe na yeyote. Wingu la woga lilitanda manthari ya pale. Ndege na wadudu walitimya ndimi zao kusubiri kitakacho jitokeza. Chumba cha wazazi wa Mutuvie, chumba cha kupikia na kile chake vyote vilikuwa milango wazi. Alitarajia watu wawili pale nyumbani, baba na mama tu. Alishangaa ni nani mwingine anamiliki ufunguo wa chumba chake isipokuwa yeye pekee. Aliamua kuitana ili kuondoa utata uliomkumba. Sauti yake haikujibiwa na mtu wala mwangwi. Panya aliyekuwa begini mwake alitikisatikisa begi kana kwamba anaomba uhuru wa kutorokea yaliyo mbele ya kijana wetu. Mwili wa Mutuvie uliganda kwa woga. Kama mwanamume, Mutuvie alijijasirisha kufululiza hadi kwa chumba chake. Maskini kijana wetu hata kabla kuingia ndani, alipatana na damu nyingi iliyotapakaa karibu na mlango wa nyumba. Alipigwa na butwaa na kuangusha begi chini kisha akafutuka kuelekea chumba cha kupikia huku akiitana mama, mama. Karibu na mlango wa chumba cha kupikia aidha alipata damu matapishi yametapakaa pale. Ardhini palikuwa na mikwaruzo ishara kwamba palikuwa na mng’ang’ano dhidi ya viumbe wawili. Alichungulia ndani huku akiita  mama. Upande wa ndani vyombo kadhaa vilikuwa vimeanguka ovyo ovyo na maji kutapakaa kila mahali. Alikimbilia chumba cha wazazi huku machozi yanamtiririka. Kukaribia mlango wa kile chumba, mlango ulijifunga kwa kishindo. Alijaribu kuufungua huku hakiita baba na mama. Aliusukuma kwa kutumia bega lake na goti la mguu wake wa kulia lakini komeo ilikuwa ishawekwa kutoka ndani. Aliugonga  gonga kwa vishindo huku akiendelea kuita lakini hakupata jibu. Alipoangaza macho kusaka silaha ya kuvunja mlango, aliona karatasi ilioandikwa PIPA LA TAKATAKA. Fahamu zilikuwa zimemtoka lakini alijipata karibu na pipa la taka taka.Ndani ya pipa hilo hakukuwa na chochote ila jeneza lililobeba kiunzi cha mifupa ( skeleton). Kabla hajafanya lolote, kile kiunzi kilipasa sauti. “Mwanangu, mimi ni baba yako na usinikaribie…..,” “baaaa… “ ‘ usiniite!’ sauti ilikatiza kijana wetu. “ Niko tayari kukutoa kafara lakini kwanza enda zizini umsalimie mama yako. Harrakisha! Sauti iliendelea. Mutuvie alijihisi ahera. Ile sauti ilimtia gia ya hadi zizini. Zizini alipata kiunzi kingine cha mifupa. Alianza kwenda kisengesenge lakini sauti ilimwita. “Mutuvie mwanangu mbona waniondokea? Mimi ni mama yako usiogope.” Miguu ya Mutuvie ilikufa ganzi na akazirai. Akiwa pale chini kile kiunzi kilinyosha mkono juu yake na kusema.”LALA SALAMA.”

Mutuvie aligutushwa na mlio wakitanda. Alijipata amelala mvunguni mwa kitanda na juu yake gondoro limeandikwa LALA SALAMA. Juu ya kitanda ni mgeni wake Winnie aliyekuwa amemtembelea  usiku wa kuamkia siku hiyo. Alipotazama akrabu ya saa ukutani,ilikuwa saa moja na dakika ishirini asubuhi. Alikuwa amechelewa kunywa dawa ya asubuhi kwa dakika ishirini. Alikimbilia begi lake la rangi ya udongo liliyokuwa kochini na kulifungua kwa makini. Alitoa kidonge cha dawa na kukibwagia kinywani. Alikimeza bila ya maji na kuangaza macho yake kitandani.Mgeni wake alikuwa  angali amelala fofofo. Ametia mguu wake mmoja kwenye mini sketi yake ya samawati. Kanchiri nyekundu ilikuwa chini karibu na kochi nayo blausi yake nyeupe iko juu ya kochi.” Kitandani nilitoka lini? Labda mototo wa wenyewe aliniskia niking’ang’ana na ndoto zangu mle mvunguni? Kweli nilitoa usaidizi alioutaka mgeni wangu Winnie?” Mutuvie alianza maswali.

HADITHI YA KUSISIMUA

ANN NA MUTUVIE Jina lake ni Ann. Sura anayo ndio, umbo analo ndio pia tabasamu lake lingemvutia kila mtu kwenye gari waliyoisafiri. M...